MICHAEL ALITUAMSHA TUKAENDELEA KULALA. _________________________ Mwaka 1983,
Wakiwa kwenye hatua za mwanzo za utayarishaji wimbo huo, Quincy akabaini uhitaji wa kitu kipya muhimu kulingana na maudhui ya wimbo husika. Alichofanya ni kumshauri Michael kuongeza kionjo kitakachoupa uzito ujumbe kusudiwa wa wimbo huo.
Wimbo huo wa Liberian Girl unamzungumzia msichana mrembo wa Kiafrika kutoka nchini Liberia ambaye Michael alionesha kuvutiwa naye kimapenzi na hivyo kukaa chini na kuandika mashairi ya kueleza hisia alizonazo juu yake.
Ili kuonesha jinsi Michael 'alivyokufa' kwa msichana huyo, Quincy akamwambia kwamba itapendeza zaidi kama ndani ya wimbo huu yatazungumzwa maneno japo machache ya lugha inayozungumzwa nyumbani kwa msichana huyo, (barani Afrika).
Michael akaonesha kuguswa sana na idea ya Quincy, haraka sana akamwambia afanye kitu hicho ambacho aliona dhahiri kitaufanya wimbo wake kuwa wa kipekee sana. Quincy akamwambia Michael "limekwisha hili.!
Haraka, Quincy akatafakari... Je, ni lugha ipi ikitumiwa itaonesha utambulisho wa msichana kutoka Afrika ? Kiswahili kikawa ndilo jibu sahihi kwake, akaamua kutumia maneno machache ya Kiswahili kwenye kionjo hicho.
Lakini Quincy hakuishia hapo, akataka maneno hayo yatamkwe na mwanamke kutoka barani Afrika, chaguo lake likaangukia kwa mwanamuziki mahiri wa Jazz kutoka nchini Afrika Kusini, mwanamama Letta Mbulu.
Letta ambaye alikuwa akivuma sana enzi hizo kama mmoja wa wanamuziki mahiri wa Jazz kutoka barani Afrika, akashirikiana na mumewe , Caiphus Semenya, jinsi ya kuyaweka maneno machache ya Kiswahili katika wimbo huo.
"Nakupenda pia... Nakutaka pia.... Mpenzi weee..!!" Maneno machache ya Kiswahili, yakatamkwa na Mwanamama Letta Mbulu katika kibao cha Liberian Girl na kukipa kibao hicho kionjo cha kipekee cha lugha ya Kiswahili.
Wimbo ukakamilika. Mnamo tarehe 31 ya mwezi Agosti 1987, Michael Jackson akaachia albamu yake ya Saba kutoka Studio iitwayo "Bad". Wimbo wa "Liberian Girl" ukawa moja ya nyimbo Bora kabisa zilizomo kwenye albamu hiyo.
Unaweza kujiuliza, iweje Quincy achague kutumia Kiswahili kumzungumzia msichana kutoka Liberia, wakati lugha hiyo hata nchini humo haizungumzwi ? Jibu ni kwamba, Kiswahili kilianza kuonekana kama lugha ya Afrika, wakati wenyewe tukiwa hatuna habari nacho.
Hakuna yeyote aliyelitazama jambo hili katika jicho la fursa. Wenye mamlaka ya Kiswahili hawakuweza kabisa kuona fursa iliyopo kwa Gwiji wa muziki duniani Michael Jackson kutumia lugha ya Kiswahili kwenye tungo iliyopelekea albamu hiyo kuwa moja ya albamu bora za muda wote.
Ni kama Michael na Quincy walituamsha usingizini, lakini wenye Kiswahili chetu tukaendelea kulala usingizi wa Pono kwa kushindwa kutumia 'opportunity' hiyo kukitangaza Kiswahili duniani kupitia Michael Jackson huyo huyo na wimbo wake huo.
"Liberian Girl" ingeweza kutumika kama chachu ya kukitangaza Kiswahili kimataifa. Tayari Michael alishaingia mwenyewe kwenye 18 zetu, nasi tungepita humo humo kukitangaza Kiswahili chetu, Wallah inawezekana leo tungekuwa mbali sana.!
Takwimu zinaonesha mpaka sasa, Kiswahili hakipo katika lugha 10 zinazozungumzwa zaidi duniani, na kwa Afrika, Kiswahili kinashika nafasi ya Nne katika lugha za ndani za Afrika zinazozungumzwa zaidi, kikitanguliwa na lugha za Hausa, Yoruba, na Igbo kutoka nchini Nigeria.
Katika uso wa dunia, lugha ya Kiingereza ndiyo kinara zaidi kuzungumzwa, ikifuatiwa na lugha ya Mandarin kutoka China, huku Kihindi kikichukua nafasi ya tatu kwa kuzungumzwa na watu wengi zaidi ulimwenguni.
Nafasi ya Nne inashikiliwa na Kihispania, ya Tano ikishikiliwa na Kiarabu, huku Kifaransa kikishika nafasi ya Sita kwa kuzungumzwa zaidi. Nafasi ya Saba ni Kibengali kutoka Bangladesh, nafasi ya Nane ni Kireno.
Nafasi ya Tisa ni lugha ya Kirusi kutoka Russia, huku nafasi ya Kumi ikishikiliwa na lugha ya Ki Urdu kutoka nchini Pakistan. Takwimu hizi ni kwa mujibu wa mashirika mbalimbali ya kitafiti yanayoshugjulika na tafiti za maendeleo ya lugha ulimwenguni
Japo vipo vigezo vingi vinavyopelekea lugha fulani kuzungumzwa zaidi duniani kuliko lugha nyingine, lakini baadhi ya wenzetu hutumia fursa au hata ujasusi mkubwa katika kukuza tamaduni zao zikiwemo lugha za makabila yao.
Kwetu "Liberian Girl" lilikuwa bonge la bao ambalo kama tungelitazama kwa jicho la fursa tangu nyakati hizo tungekuwa mbali sana. Michael alitusanua, Waswahili tulivyo jeuri tukakataa kumshobokea na kuendelea kuuchapa usingizi.
Makala nyingine zinazocheza na ladha yako
Mapendekezo haya yanatokana na kile unachosoma sasa + Endelea kugundua zaidi
Maoni