SARE YA SIMBA YA JANA INA THAMANI KULIKO INGESHINDA.???
Hatimae jana tambo za Dabi zilipata majibu kwa timu za Simba na Yanga kutoka suluhu ya bila kufungana(0-0). Kwa maana hiyo timu zote ziliambulia pointi moja moja.
Mchezo wa jana pamoja na matokeo kuwa suluhu umetupa picha nyingi za Dabi. Kwamba Dabi ni harakati na mbinu zaidi ya uwezo wa kucheza soka uwanjani. Kwamba kumbe kama Simba asingepelekwa Gwantanamo na waamuzi wasingetoka Hamelini ni wazi tena bila kificho kwamba Simba angeibuka na ushindi mnono.
Nimefurahishwa sana jana nilipobaini kuwa mashabiki, wapenzi na wadau wa soka wanaojitambua na wasiokuwa na roho mbaya na bila kujali wao ni wa upande wa Simba au Yanga waliongea lugha moja tu kuwa katika mechi hiyo Simba alicheza mpira safi, alitawala mchezo, na walistahili ushindi.
Linapokuja swali kuwa ni kwanini basi pamoja na kutawala mchezo Simba hawakupata ushindi, hapo ndipo tunapoangukia kwenye majibu mengi tofauti. Moja ya majibu ambayo ndiyo yalikuwa maoni ya wengi lilikuwa ni jibu la Mwamuzi au waamuzi. Ni kweli kuwa kuna namna haikuwa sawa katika kulikataa goli la Suleiman Mwalimu wa Simba. Unapolikataa goli ambalo uwanja mzima unaliona ni goli halali unakuwa unaiathili kisaikolojia timu husika; kwamba wachezaji wake wanajiona kumbe wanafanya kazi bure hata wakifunga tena goli linaweza likataliwe.
Tabia hii ya waamuzi kuamua matokeo ya michezo ya ligi haikuanza jana wala juzi, tabia hii imekomaa. Tunaweza kudhani tuna mabingwa au washindi wa halali wa michezo; kumbe sivyo. Nilidhani adhabu kali zaidi ziendelee kutolewa kwa waamuzi wanaoharibu mpira. Ni kweli kuwa ukishakoseshwa ushindi na mwamuzi hata yeye akiadhibiwa wewe uliyepoteza hupati kitu, lakini ni vizuri adhabu ikawa kubwa kiasi kwamba wewe mwamuzi na aliyekukodi mkae muijutie. Wengine wakiona mwenzao amefungiwa miaka 5 na adhabu ya milioni 10 hawatathubutu kununuliwa na kupoteza kazi na taaluma yao. Bila kufanya hivyo, kila siku wanyonge watakuwa wanaonewa.
Tukiachilia mbali Dabi na makandokando yake, niwatahadhalishe Simba kuwa kuanzia sasa wamejipalia mkaa. Katika michezo yao ijayo wajiandae kuwa hawatakuwa wanacheza na timu moja. Kama walivyokuwa makini Zanzibar akina Magori waendelee hivyo hivyo na ufuatiliaji katika viwanja vyote. Kama yaliyofanyika kwa Dodoma jiji ndiyo yeleyele yamefanyika Zanzibar, basi hayohayo watataka yafanyike Mkwakwani, Majaliwa na kwingineko.
Juu ya tahadhali hiyo, kwa viongozi, wapenzi na mashabiki wa Simba, chonde chonde tuwalinde wachezaji wetu. Mlindeni Chama, mlindeni Luemba, mlindeni Geuye, mlindeni Mpanzu, mlindeni Kapombe, mlindeni Rushine, mlindeni Kibabage, mlindeni Mwalimu, mlindeni Aoura, mlindeni Kassali, mlindeni Toure na walindeni wengine wote. Wale jamaa wameshajua kuwa timu hii inakuja kuwa tishio na habari ya mjini. Zitatumika kila hila kuwapoteza wachezaji hawa katika anga la soka nchini. Watapondwa kwenye mitandao, watasakamwa na vyombo vya habari, wataalikwa kwenye viwanja vya starehe, watazushiwa mambo chungu nzima, watalogwa, watapelekewa mijimama, watashawishiwa kwa pesa waisaliti timu n.k. Bila umakini wa ulinzi hii timu haitadumu hadi mwisho wa msimu. Tutawaona na hawa hawafai na tutasajili wengine wapya.
Sare ya Simba imetusaidia sana kujitambua na kutupa hamasa ya kutenda zaidi. Imetuondolea mawazo ya kuamini kuwa timu imeshakamilika hivyo hatuhitaji nguvu na umakini zaidi. Tungeshinda jana tungetawaliwa na njozi za ubingwa na kujikuta kesho tutastukizwa na kufungwa kizembe na akina TRA, Mbeya city na wengineo. Ni vizuri jana imenyesha na tumepaona panapovuja. Sasa tuzibe na tusilibe kabisa.
Tusijidanganye kuwa kutoa sare Gwantanamo wenyewe wamefurahi; laxima nao wanakwenda kujipanga upya. Usikute mechi ijayo tukapelekwa gereza jingine moto zaidi la Black Dolphin, CECOT, au tukaletwa hapa hapa jirani Ukonga kama danganya toto ili tujisahau tujilegeze watufunge. Mwendo uwe ni uleule wa man to man hadi kieleweke.
Pongezi nyingiii kwa wachezaji waliopambana, pongezi kwa kocha Barker kwa jitihada zake ndani ya kipindi kifupi, pongezi maalum kwa Mwenyekiti wa Bodi kwa usimamizi mzuri wa timu, pongezi kwa mashabiki na wapenzi wa Simba waliovuka maji kuhakikisha wachezaji hawawi wanyonge Zanzibar; na pongezi kwa wote waliobaki kwa maombi na michango yenu ya hali na mali. Hii ngoma bado kabisa. Haijaisha na haiishi mpaka iishe.
MUNGU IBARIKI SIMBA.
Makala nyingine zinazocheza na ladha yako
Mapendekezo haya yanatokana na kile unachosoma sasa + Endelea kugundua zaidi
Maoni