AMIRAH WANGU Sehemu ya 01
Tunaanza...
Asubuhi na mapema, Sheikh Abdullah alimuita binti yake, Amirah, ambaye alikuwa na umri wa miaka ishirini na tatu. Amirah alitoka chumbani kwake na kumfuata baba yake ili kumsikiliza. "Baba, mimi huyu hapa," alisema Amirah, binti mwenye heshima. Alikuwa amevaa vizuri, kama binti wa Kiislamu.
"Kaa hapa binti yangu," alisema Sheikh Abdullah huku akimwonyesha mahali pa kukaa kwenye sofa. Amirah alikaa na kumtazama baba yake. Muda mfupi baadaye, Bi. Sauda, mke wa Sheikh Abdullah na mama mzazi wa Amirah, aliingia ndani. Alikuwa akitoka kufanya usafi uani.
"Mke wangu, bora umefika, nilikuwa nataka kuongea na binti yako kuhusu lile jambo," alisema Sheikh Abdullah.
"Ongea naye, mimi bado nina kazi," alisema Bi. Sauda. Bila shaka alijua jambo ambalo mumewe alitaka kumuambia binti yake.
"Sawa."
Sheikh Abdullah alimwangalia binti yake kwa tabasamu.
"Hakuna kitu nachokifurahia kwa sasa kama kuona bado unaendelea na maadili binti yangu. Mwenyezi Mungu amefurahishwa sana na kitendo chako cha kuwa karibu naye. Ukiendelea hivi, Allah hatakuacha binti yangu."
"Amina, baba," alijibu Amirah kwa upole huku akiwa amejisitiri.
"Nilikuwa napenda kukuambia kuhusu chuo. Huendi tena Dodoma. Tumeona usomee tu hapa Dar es Salaam binti yangu, lakini utakuwa unaishi huko chuoni, ili uendelee kufanya vizuri zaidi. Hiyo kozi yako ya uuguzi inahitaji umakini mkubwa. Ujikite kwenye masomo vizuri. Ukiwa hapa nyumbani, aaaaah, utakuwa unajichanganya.
Mara sijui upike, mara vile, mimi sipendi kabisa. Kuna chuo kipo hapa Dar tu, ni kizuri sana na kinakufaa," alisema Sheikh Abdullah.
Amirah alifurahi sana.
Alipenda sana kuwa karibu na familia yake. Dodoma ilikuwa mbali sana. Alisomea huko kwa miaka miwili, na sasa alikuwa anaenda kumaliza miaka miwili mingine hapa Dar. Kwake, hii ilikuwa furaha maana hata akipatwa na shida yoyote, itakuwa rahisi kupata msaada wa familia.
"Baba, asante sana, ninafurahi kusikia hivyo. Kaka Muhammad amekubaliana na hili?" alihoji Amirah kwa furaha.
"Ndio, amekubali bila shida. Na mdogo wako Fatma wa darasa la saba anaenda shule ya bweni."
"Kwanini baba? Mimi naona si sahihi kabisa. Shule ya bweni kuna mambo mengi sana, halafu Fatma bado mdogo. Akae kwanza hapa, aanze bweni akiwa kidato cha kwanza," alishauri Amirah.
Sheikh Abdullah alikaa kimya kwa muda kisha akajibu, "Lakini ni kweli. Subiri niongee na mama yako kwanza." Maisha ya familia hiyo yalikuwa ya kawaida kabisa. Sheikh Abdullah alikuwa baba wa watoto watatu: wa kwanza Muhammad, wa pili Amirah na wa tatu Fatma. Alikuwa na mke mmoja tu. Muhammad, ambaye ndiye mtoto wa kwanza, alikuwa ameajiriwa serikalini na alikuwa na kazi nzuri tu.
Amirah ndio hivyo, alikuwa amebakiza miaka miwili amalize chuo. Ilikuwa ni familia iliyoshika dini sana.
Majira ya mchana, familia ya Mzee Stephen pamoja na Bi. Anna walikuwa wakipata chakula pamoja na vijana wao wawili, Treson na Joshua. Familia hii ilishika dini sana.
Stephen alikuwa mchungaji wa kanisa la Methodist, kanisa maarufu sana nchini Tanzania. Alijulikana kama Mchungaji Stephen.
"Nimesema kesho, kuna mfungo. Hivyo kila mtu ajiandae kufunga kabisa. Ni familia nzima, wala sitaki kuletewa visingizio hapa, mpaka huyo Fadhila atafunga," alisema Mchungaji Stephen. Fadhila alikuwa mfanyakazi wa ndani.
"Baba, mimi nitakuwa na zamu ya usiku kesho, nipo tayari kabisa
kufunga, wala sina kizuizi," alisema Joshua kisha akamtazama mdogo wake Treson, ambaye alikaa kimya bila kuongea chochote.
Ukimya wake uliwafanya kila mmoja amtazame.
Baada ya muda, Mchungaji Stephen aliongea tena. "Treson, wiki ijayo unarudi chuoni, huu ni mwaka wako wa mwisho kabisa. Pambana kijana wangu ili ulete matokeo mazuri. Kaka yako alikataa kufanya mambo ya biashara, alisema kuwa si mambo yake, hivyo nakutegemea sana wewe. Wewe una upevu kabisa na haya mambo. Mimi natakiwa kukaa chini kufanya kazi ya Mungu, na si kuendelea na mambo haya tena."
"Usijali baba, nimeenda kupigania kampuni yetu. Nategemea mambo yataenda sawa bila shida."
"Asante kijana wangu, ni kukutakia tu
masomo mema. Kumbuka mwaka huu ndio wa mwisho. Pambana sana," alisema Mchungaji Stephen, na Bi. Anna akaingilia kati kwa pupa.
"Mambo ya wanawake achana nayo. Kumbuka kanisani kwetu kuna mabinti wengi wazuri wanamuamini Yesu kuwa Bwana na Mwokozi wa maisha yao. Ukimaliza tu chuo, utakuja kuoa. Achana na hao wa huko chuoni wanapenda tu kuchuna hela. Halafu wewe ni mtoto wa mchungaji, inatakiwa uoe vizuri, siyo kwa njia za panya."
"Nimekuelewa mama."
"Mama bwana! Unadhani Treson ni mdogo? Anaelewa kila kitu, ni mtu mzima huyo. Miaka ishirini na saba bado mdogo? Hayo maneno si ya kumuambia," alisema Mchungaji Stephen.
"Mtoto ni mtoto tu, lazima aambiwe."
Majira ya usiku, familia nzima ya
Mchungaji Stephen walikusanyika kufanya ibada ya usiku. Aliyekuwa mhubiri alikuwa Joshua. Ibada ilienda sawa kabisa, walimaliza na kila mmoja alienda chumbani kwake kulala.
Treson alikuwa bize na kompyuta yake akisoma mtandaoni. Licha ya kusoma chuo kikuu, bado aliona ni vyema kuelimika zaidi mtandaoni pia.
Upande mwingine, Amirah alimpigia simu rafiki yake kipenzi sana, Charline, na kumuambia kuhusu ratiba yake kubadilishwa chuo. Charline alifurahi sana. Wote walichukua kozi moja
lakini walitengana baada ya Amirah kwenda kusomea Dodoma.
Basi Amirah alichukua fomu mtandaoni ya chuo alichoambiwa na baba yake, na akatuma maombi yake. Asubuhi na mapema, aliamka na kuangalia kama amejibiwa. Alikuta amejibiwa na amepewa maelezo yote. Aliambiwa anatakiwa kuripoti chuoni mapema ili kuweka mambo mengine sawa.
Alimuambia kaka yake Muhammad kila kitu na alimuomba pesa ya kununua baadhi ya vitu, kama viatu na mahitaji mengine ya msingi. Jioni alitumiwa pesa na kaka yake. Kesho kutwa alienda kununua vitu vyake. Ilikuwa imebaki siku mbili tu aende chuoni. Ilikuwa kama bahati kwake kupata nafasi kwenye chuo hicho cha CCAP UNIVERSITY.
Baada ya siku hizo mbili, Amirah alijiweka sawa. Aliagana na familia yake. Kaka yake alikuwa bize sana siku hiyo hivyo hakuweza kwenda kumsindikiza mdogo wake. Alimpa tu pesa ya nauli na matumizi.
Muhammad ndiye aliyekuwa kila kitu kwa mdogo wake Amirah.
Chuo kilikuwa mbali kidogo na nyumbani kwao, kama masaa matatu hivi kwa gari, lakini ilikuwa ndani ya Dar es Salaam. Majira ya saa tisa, alipanda bajaji mpaka stendi na kupanda basi kuelekea chuoni.
Aliwasiliana na rafiki yake na kumuambia kuwa anaelekea chuoni. Charline alimwambia kuwa yeye tayari alikuwa chuoni, alifika asubuhi. "Natamani kukutana na wewe tena Charline, baada ya siku nyingi hivi, si mwaka?" alihoji Amirah. "Mwaka tayari, tunaelekea miaka miwili sasa."
"Mmmh! Nimekukumbuka sana."
"Usijali, kwa sasa utakuwa unalala na mimi. Nimeletewa jina lako hapa kama mwandani wangu wa chumba, yaani ninafurahi sana," alisema Charline.
Amirah alifurahi mno na hakutaka kuamini. Alimuambia ataamini mpaka pale atakapojiridhisha mwenyewe.
Baada ya masaa matatu, Amirah alifika eneo karibu na chuo. Sio chuoni penyewe, ila chuo kilikuwa kinaonekana kwa mbali.
Gari lilifikiri alikuwa anaelekea chuoni kabisa, hivyo alitakiwa kushuka ili achukue bajaji au bodaboda. Alishusha begi moja kubwa na lingine la mgongoni.
Aliposhuka, kulikuwa ni sehemu ya upweke sana, haikuwa na mwendo wowote. Hivyo kila bajaji iliyopita ilikuwa na abiria.
Alikaa takriban nusu saa akisubiri bodaboda au bajaji. Amirah alichoka baada ya kukaa kwa muda mrefu.
Aliamua kukalia begi lake kubwa. Muda mfupi baadaye, kuna gari nzuri tu ilipita na kusimama mbele kidogo. Mtu alishuka kwenye gari, hakuwa mwingine bali alikuwa Treson. Alimfuata Amirah kwa upole, na kumuuliza swali.
"Unahitaji msaada?"
Sauti ya Treson ilimshutua sana Amirah na kumtoa kwenye dimbwi la mawazo. Aliushika moyo wake baada ya kumtazama Treson, ambaye alitamani kuendelea kuongea lakini aliganda kwa muda. Hakutarajia kabisa kukutana na mwanamke mzuri na mrembo kama Amirah. Treson alijikuta amevutiwa sana na Amirah, alishindwa kuelewa.
Itaendeleya......
Makala nyingine zinazocheza na ladha yako
Mapendekezo haya yanatokana na kile unachosoma sasa + Endelea kugundua zaidi
Maoni