MWONGOZO WA MWANZO KABISA: Jinsi Ya Kuanza Kazi Za Freelancing Mtandaoni (Tanzania)
(1) ELEWA KWANZA FREELANCING NI NINI
Freelancing ni kufanya kazi kwa wateja kupitia mtandao na kulipwa kwa kazi unayofanya, si kwa kuajiriwa ofisini. Unaweza kufanya kazi ukiwa nyumbani, kijijini au mjini, mradi una simu au kompyuta na intaneti.
Hakuna uchawi wala miujiza. Ni kazi halali kama kazi nyingine zote, tofauti ni kwamba unajitegemea. Inahitaji muda, subira na kujifunza hatua kwa hatua, si kukurupuka.
(2) FAHAMU WEBSITE ZA KAZI ZA MTANDAONI
Kuna website maalum zinazounganisha wateja wanaohitaji kazi na watu wanaojua kufanya kazi hizo. Hizi website ndizo msingi wa freelancing.
Ndani yake, mteja anaweka kazi, na wewe unaomba au unaweka huduma yako kulingana na mfumo wa website husika. Ndipo kazi nyingi za mtandaoni zinapatikana.
(3) – WEBSITE KUBWA NA YA KITAALAMU
Upwork ni website kubwa na rasmi zaidi. Wateja huweka kazi, kisha wewe unaomba kazi hiyo. Mwanzo ni ngumu kidogo kwa sababu ushindani ni mkubwa, lakini ukishapata kazi hata moja au mbili, akaunti yako inaanza kuaminika. Upwork inalipa vizuri na inafaa kwa mtu anayepanga freelancing iwe kazi ya muda mrefu.
(4) FIVERR – RAHISI KWA MWANZO KABISA
Fiverr ni tofauti kidogo. Hapa hauombi kazi, bali unaweka huduma zako wazi. Mteja ndiye anakutafuta. Fiverr ni rahisi sana kwa wanaoanza kabisa kwa sababu huna presha ya kuandika maombi mengi. Hata hivyo, mwanzo malipo huwa madogo mpaka ujijenge, upate wateja na review.
(5) FREELANCER.COM – MAZOEZI YA MWANZO
Freelancer.com inafanana na Upwork lakini ni rahisi kidogo kuanza. Unagombania zabuni (bid) kwenye kazi zinazowekwa. Kuna kazi nyingi ndogo ndogo, hivyo ni sehemu nzuri ya kujifunzia mfumo wa freelancing na kupata uzoefu wa mwanzo.
(6) PEOPLEPERHOUR – KAZI NDOGO NA ZA HARAKA
PeoplePerHour inafaa kwa kazi ndogo ndogo na za haraka, hasa graphic design, writing na kazi za kidigitali. Sio maarufu sana Afrika lakini inalipa na inafanya kazi. Ni chaguo la ziada kwa mtu anayeshapata uzoefu kidogo.
(7) JIUNGE KWA UTAHADHARI (USIKIMBILIE ZOTE)
Usijiunge na website zote kwa wakati mmoja. Anza na moja au mbili tu ili usichanganyikiwe. Kujiunga kunahitaji email, jina lako halisi, picha ya kawaida bila filter, na maelezo mafupi kuhusu wewe na kile unachoweza kufanya.
(8) ELEZA UNACHOWEZA, SI UNACHOKOSA
Usiandike kuwa huna uzoefu. Badala yake, eleza kile unachoweza kufanya hata kama ni kidogo. Unaweza kuandika kwa Kiswahili, kutengeneza poster kwa Canva, kutafsiri, kuandika maandishi, kuingiza data au kutengeneza CV. Kila freelancer aliwahi kuanza bila uzoefu.
(9) CHAGUA KAZI MOJA YA KUANZIA
Usiruke ruke kufanya kila kitu. Chagua kitu kimoja kwanza. Kama unajua Canva, anza na poster na social media posts. Kama unajua kuandika, anza na writing au typing. Kama una simu tu, anza na data entry au kazi rahisi. Kazi ndogo hukusaidia kuelewa mfumo, kupata review ya kwanza na kujenga ujasiri.
(10) JINSI YA KUPATA KAZI YA KWANZA
Kazi ya kwanza ndiyo ngumu zaidi. Inaweza kuchukua wiki au hata mwezi. Usikate tamaa. Kwenye Upwork au Freelancer, soma kazi vizuri, andika maombi mafupi na ya kueleweka. Usiseme unaomba kazi, eleza namna utakavyomsaidia mteja. Kwenye Fiverr, weka picha nzuri ya huduma, eleza kwa lugha rahisi na anza na bei ndogo ili kuvutia wateja wa mwanzo.
(11) MALIPO NA USALAMA WA PESA
Website hizi hulipa kupitia PayPal, Payoneer au benki. Kwa Watanzania, Payoneer inafanya kazi vizuri zaidi. Usikubali kulipwa nje ya website mwanzo, hata kama mteja anaonekana mzuri. Hapo ndipo watu wengi hupigwa pesa.
(12) YOUTUBE NI DARASA LAKO LA KILA SIKU
Kwa mwanzilishi, YouTube ni chuo. Tafuta video kwa kuandika maneno kama: How to start freelancing for beginners, How to get first job on Upwork, Fiverr tutorial for beginners, Canva design for beginners, au Online jobs for beginners. Tafuta video zinazoonyesha screen, zinaeleza hatua kwa hatua na zina maoni mengi mazuri. Epuka video za “get rich quick”.
(13) HITIMISHO
Freelancing si miujiza wala bahati ya siku moja. Ni kazi ya kujifunza, kujaribu, kukosea na kurekebisha. Usijiulize utapata lini pesa, jiulize umejifunza nini leo. Ukijifunza kila siku, pesa itakuja yenyewe.
Makala nyingine zinazocheza na ladha yako
Mapendekezo haya yanatokana na kile unachosoma sasa + Endelea kugundua zaidi